Ndugu Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza,

Ndugu wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa,

Mhe. Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana,

Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza,

Ndugu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,

Ndugu Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza,

Ndugu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Bugando,

Waheshimiwa Madiwani mliopo hapa,

Ndugu Mkurugenzi wa kiwanda cha kuzalisha dawa,

Waandishi wa habari,

Wageni waalikwa,

Mabibi na Mabwana.

 

Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kwa kutuwezesha kufika katika siku ya leo tukiwa wazima na wenye afya tele.

Vilevile nichukue nafasi hii kuupongeza uongozi wa Prince Pharmaceutical, kwa kuwa na wazo la kuwekeza katika mkoa wetu wa Mwanza, sisi kama wana Mwanza tunaona dhamira yetu ya kuvutia wawekezaji wengi sasa inatimia kwani mtakumbuka ni hivi karibuni tulikuwa na kongamano kubwa kabisa la uwekezaji kwa kanda hii ya ziwa, mkoa wa Mwanza ukiwa ni mwenyeji wa kongamano hilo lililofanyika katika Hoteli ya Malaika iliyoko Mkoani hapa kwa lengo la kuvutia wawekezaji kama Prince Pharmaceuticals.

Ndugu wananchi,

Labda ni rejee kidogo

alichokisema Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Mohamed Gharib Bilali katika hotuba yake ya Ufunguzi wakati wa kongamano hilo, kwamba “nia ya Serikali ni kuweka mazingira mazuri na ya kuvutia na  kuona watu wengi wanakuja kuwekeza katika kanda hii”. Sasa hili ambalo ndugu zetu wa Kings Pharmaceutical, mmelifanya ni moja ya matunda hayo, mazingira ni mazuri, fursa za kibiashara zipo na hali ya Ulinzi na Usalama ni ya kuridhisha ndio maana mkapata msukumo wa kuja kuwekeza. Hongereni sana.

Ndugu wananchi,

Katika mkoa wa Mwanza na kanda ya Ziwa kwa ujumla, kwa muda mrefu tumekuwa hatuna kiwanda cha kutengeneza dawa katika eneo letu. Hali hii imefanya Kanda ya ziwa kutegemea dawa kutoka sehemu zingine kama vile Dar es Salaam na nje ya nchi, jambo ambalo limeongeza gharama sana kwa serikali na hata wananchi wanaofanya biashara ya dawa kwa ujumla wao, vile vile kutokuwepo na kiwanda kumekuwa kukiathiri  upatikanaji wa dawa kwa wakati katika vituo vyetu vya kutolea huduma za Afya. Hivyo ni imani yangu kwamba, uwepo wa kiwanda hiki kitakuwa mkombozi kwa mkoa wetu wa Mwanza na wananchi wa kanda ya ziwa kwa ujumla hasa ukizingatia kuwa, Mwanza imekuwa kitovu cha biashara kwa nchi za maziwa makuu.  

 

Ndugu wananchi,

Pengine sasa tuone faida za kuwepo kwa kiwanda hiki katika mkoa wetu wa Mwanza. Tumeelezwa kuwa kiwanda kitakuwa na seksheni nne (4) za uzalishaji dawa yaani seksheni ya utengenezaji wa dawa za maji (syrup), Malai (ointments), poda (powder), na viambukuzi (antiseptics). Ambazo zote hizi zitatoa ajira kwani tunajua fika Idadi ya wakaazi wa Mkoa wa Mwanza kwa sasa wapatao Milioni 2.7 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012, na ongezeko la wananchi wetu kwa kiwango cha asilimia 3% kwa mwaka, ni ushahidi tosha kwamba serikali na wadau wengine wanayo dhima ya kuhakikisha ongezeko hilo linakwenda sambamba na upatikanaji wa ajira. Sasa basi, wenzetu wa Prince pharmaceutical, wametuonesha kwa vitendo kwa kuanzisha kiwanda hiki, ambacho baada ya kuanza kazi kitakuwa na uwezo wa kuajiri wafanyakazi wapatao 50 hadi 100 lakini mbali na ajira hizo, katika uchumi kuna kitu kinaitwa multiply effect ambapo, uwepo wa kiwanda kutasaidia kuongeza kipato cha mtu mmojammoja, mapato kwa serikali ambayo yatasaidia mkoa wa Mwanza kuongeza ukuaji wa kasi ya uchumi na kuchangia katika pato la Taifa ambalo Mwanza kwa sasa inashika nafasi ya pili katika uchangiaji wa pato la Taifa. Ni imani yangu kuwa Kiwanda hiki si tu kitazalisha ajira ajira, bali kitakuwa mstari wa mbele katika kufanya shughuli mbalimbali za kijamii (Coperate Social Responsibility) ambazo pia zitainufaisha jamii inayozunguka kiwanda hiki.

 Ndugu wananchi,

Pamoja na nia nzuri ya kuanzishwa kwa kiwanda hiki, napenda nisisitize na kutoa tahadhari ifuatayo. Katika uzalishaji wenu wa dawa, tafadhali kumbukeni kuwa wananchi wetu ni masikini sanalakini pamoja na umasikini wao wanahitaji kuwa na afya bora ili waweze kufanya shughuli za kujiletea maendeleo. Kwa hali hiyo, hakikisheni mnatengeneza dawa ambazo zina ubora unaotakiwa lakini kwa bei ambayo hata mwananchi wa kawaida anaimudu. Najua, kama kiwanda mtahitaji kupata faida, lakini utengenezaji wa faida hiyo usiwaumize wananchi kwa kuwatengenezea dawa zisizo na ubora (dawa feki) ama kuwauzia wananchi dawa zilizopitwa na muda wa matumizi (expired) kwa kuwabadilishia lebo za tarehe za kuisha kwa muda wa matumizi ya dawa hizo.

 Tumearifiwa hapa kwamba wenzetu hawa wa Prince Pharmaceutical watazalisha dawa zao kwa kufuata viwango vya kimataifa vya ubora (Good Manufacturing Practices –GMP), rai yangu ni kwamba jambo hilo ni jema na liwe kwa vitendo.  Tunajua upo ushindani wa kibiashara kwenye soko kutoka ndani na nje ya nchi, lakini ni imani yangu kwamba mkizalisha dawa zenye ubora na mkaziuza kwa bei nzuri, mtaweza kushinda ushindani kwenye soko, maana waswahili husema …..“kizuri chajiuza, kibaya chajitembeza”.

Aidha, napenda nichukue fursa hii kuwaagiza Mamlaka ya chakula na dawa nchini (TFDA) kuhakikisha ubora na viwango vinafuatwa kwa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika kiwanda hiki kwani hivi karibuni tumeshuhudia matukio ya uwepo wa dawa bandia, sasa hatutaki hiyo itokee katika mkoa wetu.

Ndugu wananchi,

Ulinzi wa kiwanda hiki ni muhimu sana, rai yangu kwa wananchi wa maeneo haya  na Mkoa wa Mwanza kwa ujumla, ni lazima tuelewe ulinzi wa  kiwanda hiki  ni wetu sote, asitokee mtu miongoni mwetu mwenye nia mbaya ya  kuhujumu kiwanda hiki. Kwani kwa kufanya hivyo, tutakuwa tumemsononesha sana mwekezaji, lakini pia kurudisha nyuma jitihada za Serikali katika  kuwaletea maendeleo wananchi wake na mtawakatisha tamaa wawekezaji wengine waliokuwa na nia ya kuja kuwekeza katika mkoa wetu.

Sambamba na hilo, mwekezaji pia anapaswa afahamu kwamba ana wajibu wa kuilinda jamii inayo mzunguka hususani katika suala la utunzaji wa mazingira. Anao wajibu wa kuhakikisha usalama na maslahi ya wafanya kazi wake.

 Lakini kama hiyo haitoshi kwa zile ajira ambazo zinaweza kufanywa na wananchi wa maeneo haya, ni vema wakapewa kipaumbele  kwanza  na sio kwenda kuleta wageni toka nje ya nchi ili waje kufanya kazi ambazo wanajamii wa hapa wana uwezo wa kuzifanya. Wazungu wana msemo usemao (charity begins at home).

 

Ndugu wananchi,

Kabla sijamalizia hotuba yangu hii. Ninapenda kutoa wito kwa wawekezaji wengine kuiga mfano wa ndugu zetu hawa wa Prince Pharmaceutical, kwani ni ya yetu ni kuona Makampuni mbali mbali yanakuja kuwekeza katika mkoa wetu wa Mwanza. Vile vile, mimi kama mtumishi wenu wa Serikali katika Mkoa huu niwaahidi kuendelea kuwapa ushirikiano wa kutosha wakati wote na  msisite kufika ofisini kwangu pindi mtakapo ona kuna ulazima wa kufanya hivyo, nasema milango iko wazi kwangu mimi mwenyewe, lakini pia kwa wasaidizi wangu kupitia katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza.

Baada ya kusema hayo, niwashukuru tena uongozi wa kiwanda hiki pamoja na wote ambao tumekuja kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi la kiwanda hiki cha Prince Pharmaceuticals.

ASANTENI KWA KUNISIKILIZA.

 

 

 

 

 

 

 
Axact

Post A Comment: