DR. MVUNGI.
Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba aliyekuwa akipatiwa matibabu nchini Afrika Kusini amefariki dunia.

 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Bw. Assaa Rashid jana jioni (Jumanne, Novemba 12, 2013), Dkt. Sendongo Mvungi alifariki majira ya saa 8:30 mchana kwa saa za Afrika ya Kusini akiwa katika Hospitali ya Milpark.

 

“Kwa masikitiko makubwa, Tume inawafahamisha wananchi kuwa Mjumbe wake, Dkt. Sengondo Mvungi aliyekuwa akipata matibabu katika Hospital ya Milpark iliyopo jijini Johannesburg nchini Afrika Kusini amefariki dunia jana (Jumanne, Novemba 12, 2013) saa 8:30 mchana kwa saa za Afrika ya Kusini,” amesema Bw. Rashid katika taarifa yake fupi ya awali na kuongeza:

 

“Taratibu za kuusafirisha mwili wa marehemu kutoka nchini Afrika Kusini kuja nchini kwa mazishi zinaendelea na taarifa zaidi zitatolewa leo (Jumatano, Novemba 13, 2013),” aliongeza.

 

Marehemu Dkt. Mvungi alisafirishwa siku ya Alhamisi, Novemba 7, 2013 kwenda nchini Afrika Kusini kwa uchunguzi na matibabu zaidi akitokea Kitengo cha Mifupa Muhimbili (MOI) aliokuwa amelazwa baada ya kuvamiwa nyumbani kwake Kibamba, wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na watu waliomjeruhi vibaya kichwani usiku wa kuamkia siku ya Jumapili, Novemba 3, 2013.

 

Katika taarifa yake, Tume pia imewaomba watanzania wote kuungana na familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Dkt. Mvungi katika kuomboleza msiba huo.

 
Axact

Post A Comment: