Serikali inapenda kuwaarifu waombaji wa nafasi za kazi kwa tangazo la tarehe 27 Novemba, 2013 wa kada za Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Udereva kuwa usaili utaanza tarehe 4 Machi, 2014 takriban katika mikoa yote Tanzania Bara na kituo cha Zanzibar.
Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma Bw. Xavier Daudi amesema hayo leo ofisini kwake wakati akiongea na baadhi ya wadau waliomtembelea kwa lengo la kufahamu masuala mbalimbali ya uendeshaji wa mchakato wa ajira serikalini. Amesema usaili huo unaoanza tarehe 4 Machi katika mikoa takribani yote nchini utahusisha jumla ya wasailiwa 6,075 wa fani za Kilimo, Mifugo, Uvuvi na udereva.  Amefafanua kuwa vigezo vya kupanga mikoa ya usaili kwa wasailiwa wa kada zisizo za maafisa vimetokana na anwani ambazo waombaji waliwasilisha katika barua zao za maombi husika ya kazi.
Daudi alibainisha kuwa kila mwombaji aliyekidhi vigezo na kuchaguliwa kwa ajili ya usaili anapaswa kwenda kufanyia usaili katika mkoa aliopangiwa kama anwani yake inavyoonyesha katika tangazo kwenye tovuti ya Sekretarieti ya Ajira, isipokuwa kwa waombaji wa mkoa wa Katavi wao wataenda kufanyia usaili mkoa wa Rukwa na waombaji waliotumia anwani za mkoa wa Singida wao watafanyia usaili mkoa wa Manyara kutokana na sababu zisizozuilika. 
Aliongeza kuwa kwa mwombaji ambae hatazingatia anwani, siku na muda aliopangiwa na kuamua kwenda mkoa mwingine tofauti na utaratibu uliopangwa ajue wazi hatasailiwa kwa kuwa ratiba na idadi ya majopo ilishapangwa kwa kila mkoa na haitabadilishwa ili kuweza kurahisisha kazi hiyo kukamilika  kwa ufanisi.
Aidha, amewataka waombaji wote wa tangazo hilo kutembelea tovuti ya Sekretarieti ya Ajira  ambayo ni www.ajira.go.tz  wao wenyewe ili kuweza kujua kiundani endapo wamechaguliwa kufanya usaili, kufahamu tarehe, mahali na muda wa kuanza usaili ili kuepuka usumbufu usiokuwa na lazima. 
Daudi aliendelea kufafanua kuwa kwa waombaji waliotumia anuani za mkoa wa Dar es Salaam kwa nafasi ambazo sio za maofisa usaili utafanyika tarehe 11 Machi, 2014. Aidha, kwa nafasi za Maofisa Kilimo, Mifugo na Uvuvi wote usaili wao utafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 10 hadi 14 Machi, 2014. 
Katibu  amewataka waombaji wote kuhakikisha pindi wanapoenda kwenye usaili wawe wamejiandaa vya kutosha ikiwemo kubeba nyaraka muhimu hususani vyeti halisi vya taaluma zao maana vitahitajika kwa ajili ya uhakiki siku ya usaili. Aidha, amewasihi waombaji wa matangazo mengine ya nafasi za kazi kuwa na subira wakati uchambuzi ukiendelea na pindi utakapokamilika wahusika watataarifiwa.
Alimaliza kwa kuwasisitiza wadau wa Sekretarieti ya Ajira kuwa pindi wanapoona matangazo ya kazi, ikiwemo kuitwa kwenye usaili au kupangiwa vituo vya kazi katika vyombo mbalimbali vya habari hususani baadhi ya mitandao ya kijamii wajiridhishe kwanza kwa kuangalia taarifa hizo katika tovuti ya Sekretarieti ya Ajira, ili kuepuka taarifa zisizokuwa za kweli ambazo zimekuwa zikitolewa nyakati nyingine na baadhi ya watu wasio waaminifu kwa lengo la kupotosha Umma.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.
Ofisi ya Rais-Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa   Umma. 21 Machi, 2014 
Kwa maelezo zaidi; wasiliana na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Kwa barua pepe; gcu@ajira.go.tz This e-mail address is being protected from spambots, you need JavaScript enabled to view it , facebook page www.facebook.com/sekretarietiajira au simu 255-687624975.
Axact

Post A Comment: