Mheshimiwa Eng. Evarist. Ndikilo - Mkuu wa Mkoa wa Mwanza

Mheshimiwa Mariam Lugaila - Mkuu wa Wilaya ya Misungwi,

Dkt. Yohana Budeba, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi,

Mkurugenzi wa Utafiti, Mafunzo na Ugani- Mifugo na Uvuvi,

Mtendaji Mkuu LITA,

Mkurugenzi Mkuu-TALIRI,

Wanahabari,

Wageni Waalikwa,

Mabibi na Mabwana.

 

Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana siku ya leo tukiwa na afya njema. Aidha, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Uongozi mziwa wa Taasisi hizi mbili za TALIRI na LITA kwa kunipa heshima ya kuweka jiwe la msingi na kufungua kituo cha mafunzo ya mifugo vilivyopo hapa Mabuki. Nimefarijika zaidi kuja hapa leo kuifanya kazi hii kutokana na kuvutiwa na utekelezaji mzuri wa miradi hii ambayo niliiona nilipotembelea kituo hiki kwa mara ya kwanza, mara tu baada ya kuteuliwa Waziri mwenye dhamana, Mwezi Januari mwaka huu. Hongereni sana kwa kazi nzuri.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, kwanza napenda kuupongeza sana Uongozi wa TALIRI na LITA kwa jitihada zao za kuongoza shughuli za Utafiti na Utoaji wa mafunzo ya mifugo katika Taasisi zetu. Sanjari nah ii, napenda kumshukuru Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH kwa kufadhili ujenzi wa majengo haya ya maabara ya nyama, Darasa na Ukumbi wa Mitihani tunayoweka mawe ya msingi leo. Pia namshukuru Mkurugenzi wa COSTECH kwa ufadhili wa mafunzo ya Shahada za Uzamili na Uzamivu kwa watafiti wetu 24 (20 MSc na 4 PhD) waliofadhiliwa/wanaofadhiliwa na Serikali kupitia COSTECH katika Vyuo vikuu tangu mwaka 2010/2011 na miradi 15 ya utafiti wa mfugo na uvuvi inayoendelea katika Taasisi zetu nchini.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, kazi ninayofanya ya kuweka mawe ya msingi na ufunguzi wa kituo hiki cha mafunzo leo hii inaashiria jitihada za Serikali katika kupanua na kuimarisha shughuli za utafiti na utoaji wa mafunzo ya mifugo hapa nchini. Kwa kutambua umuhimu huo, Serikali imeanzisha Taasisi (TALIRI na Wakala (LITA) ili kuongeza ufanisi katika utafiti na utoaji mafunzo ya mifugo hapa nchini. Aidha, uwekaji wa jiwe la msingi na ufunguzi wa jingo vimekuja wakati muafaka. Hii ni kutokana na kupanuka kwa huduma za utafiti na mafunzo ya mifugo katika mikoa yote ya Kanda ya Ziwa ya Mwanza, Mara, Shinyanga, Kagera, Geita na Simiyu ambayo kwa pamoja ina jumla ya Wilaya 32. Hii pia ni kwa kutambua kuwa idadi kubwa ya mifugo inapatikana katika mikoa hii.

 

Ndugu Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI, nimeelezwa kuwa kutokana na mabadiliko ya muundo wa Wizara na Idara zake, Kituo hiki kimehama mara mbili. Mwaka 1994 ambapo kituo kilihama kutoka Malya na kwenda Ukiliguru na mwaka 2005 kikahamishwa na kuja hapa kilipo sasa yaani Mabuki. Kwa sababu hiyo kituo hakikuwa na majengo yake wala eneo la kufanyia utafiti na shughuli nyingine pamoja na miundombinu mingine hali iliyochangia kuchelewa usimamizi wa shughuli za utafiti hadi ilipofika mwaka 2008. Nina imani kuwa baada ya hapa, Taasisi itatumia kikamilifu eneo walilopatiwa na Wizara ambalo lina ukubwa wa takribani hekta 1,000 kwa shughuli mbalimbali za utafiti wa mifugo kwa ufanisi. Hii ikiwa ni pamoja na hekta 10 zilizotengwa kwa ajili ya majengo ya Ofisi, makazi na miundombinu mbalimbali ya kiutafiti. Ni imani yangu kuwa maeneo haya na rasilimali zake zitatumika na kulindwa kikamilifu kwa maslahi ya Taifa.

 

Ndugu Mkurugenzi Mkuu, ninafahamu kuwa TALIRI inatekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya utafiti kwa fedha kutoka Serikalini kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH). Hii ni pamoja na ujenzi wa maabara ya nyama ambayo tunaweka jiwe la msingi leo na nyumba mbili za watumishi hapa TALIRI- Mabuki, kazi ambayo ilianza mwaka 2012/2013. Ninafahamu kuwa TALIRI Mabuki ilipata jumla ya Tshs. Milioni mia nne na hamsini na tano (455,000,000/=) kutoka COSTECH kwa ajili ya ujenzi wa maabara na nyumba tatu (3) za watumishi za daraja la pili. Nafahamu pia kuwa tayari jumla ya shilingi 435,959,945.00 zimekwishatolewa kwa ajili ya maabara (Tshs. 69,863,370.00 ns Tshs 270,096,575.00) kwa ajili ya maandalizi ya awali na ujenzi wa nyumba tatu (3) za watumishi za daraja la pili na nina imani zimetumika tayari kwa kazi zilizokusudiwa.

 

Aidha, nina taarifa kuwa ujenzi wa maabara umekamilika kwa asilimia 98% na nyumba umekamilika kwa zaidi ya asilimia 95%. Napenda kuwapongeza kwa mara nyingine kwa uadilifu na uwajibikaji mzuri. Nachukua fursa hii kuiomba COSTECH kumalizia sehemu ya fedha ambazo hazijatumwa kwenu ili kuweza kukamilisha ujenzi huu pamoja na kununua vifaa kwa ajili ya maabara hii.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, najua kuna changamoto za kukosa umeme, maji na vifaa vya maabara katika kituo hiki na gharama za awali zinakadiriwa kuwa shilingi milioni 21.7 kwa ajili ya kuweka umeme na maji. Niendelee kumuomba Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH atusaidie tena kufadhili katika kazi hii. Ama kwa hakika COSTECH tutawakumbuka kwa kazi nzuri waliyoifanya lakini pia wanaimarisha wajibu wao kama wadau muhimu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini. Pamoja na hilo, ninaiagiza TALIRI ifanye utaratibu wa kupata gharama halisi za vifaa na mashine muhimu za maabara hii ili iweze kufanya uchunguzi wa kisayansi inavyotakiwa. Ni wakati muafaka kwa watafiti waliopo kutumia ubunifu wa kuandika miradi ya utafiti itakayojumuisha kuimarisha maabara hii kwa ufadhili wa fedha za ndani na nje ya Tanzania.

 

Ndugu Wakurugenzi, kama sote tunavyofahamu, upatikanaji wa fedha za utafiti na vitendea kazi ni changamoto kubwa kwa Taasisi na vituo vya utafiti na mafunzo ya mifugo katika kukidhi matarajio ya wadau katika sekta ya mifugo. Gharama kubwa zinahitajika kuchunguza, kuendesha na kusimamia shughuli za utafiti na mafunzo ikiwa ni pamoja na kuhifadhi na kuendeleza koo bora za mifugo kwa wafugaji, uhimilishaji, uzalishaji wa mbegu za malisho, kufundisha wataalam wa mifugo na gharama za kawaida za uendeshaji wa kazi za kila siku kwa vituo vyetu. Pamoja na juhudi za Serikali, nawaagiza watafiti na wakufunzi waliopo kufanya juhudi kubwa za kuandika miradi na machapisho mengi iwezekanavyo kutafuta fedha na mahitaji mengine ktuoka mifuko na fursa mbalimbali zitolewazo ndani na njea ya nchi ili kupunguza utegemezi kutoka Serikali kuu.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, Kimataifa bado tunakabiliwa ba tatizo la ufugaji usio na tija kubwa huku ukilalamikiwa kutokana na uharibifu wa mazingira, migogoro na watumiaji wengine wa ardhi kama vile wakulima na wahifadhi wa wanyamapori. Wafugaji wetu bado wamezingirwa na umaskini mkubwa licha ya idadi kubwa ya mifugo nchini. Takwimu zinaonesha kuwa Tanzania ina ng’ombe milioni 22.8, mbuzi milioni 15.6, Kondoo milioni 7.0, nguruwe milioni 2.01 na kuku milioni 58. Ni kupitia tafiti nzuri takwimu zinaweza kuleta utajirisho mkubwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

 

Wageni Waalikwa, kwa sasa Wizara yetu ina changamoto ya kudhibiti/kuzuia uvamizi wa maeneo ya mashamba unaofanywa na wananchi wanaozunguka mashamba ya Taasisi zenu. Wananchi hawa huchunga mifugo shambani bila idhini nah ii inahatarisha afya na usalama wa mifugo ya Taasisi pamoja na uharibifu wa miundombinu. Ni vyema Taasisi zenu zikatafuta mbinu mbadala ya kukabiliana na changamoto hii kwa kushirikiana na uongozi wa Wilaya husika ili utatuzi huu uwe na amani.

 

Aidha, nachukua fursa hii kuagiza ukamilishaji wa upimaji na upatikanaji wa hati miliki kwa maeneo yote nchini yanayomilikiwa na Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi yakiwemo yale yaliyopo chini ya Taasisi na Vituo vyake. Kazi hii ifanywe mapema iwezekanavyo ili kupunguza migogoro iliyopo kwa sasa na ambayo inaweza kujitokeza kwa siku za usoni.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, upanuzi na ujenzi wa miundombinu ya Kituo cha mafunzo ya mifugo Mabuki ni moja ya ahadi zilizotolewa na Serikali Bungeni kupitia Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi. Hivyo napenda kuwajulisha kuwa ahadi hiyo tunaitekeleza na tutaendelea kuzitekeleza kwa kadri fedha zitakavyopatikana. Hata hivyo, ni vyema kuwakumbusha kuwa miundombinu ya majengo hugharimu Serikali fedha nyingi. Hivyo basi ningependa kuwaasa muendelee kuitunza miundombinu hiyo ili iweze kutumika kwa muda mrefu kwa malengo yaliyokusudiwa.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa na Wageni waalikwa, kwa muda mrefu Serikali kuu imekuwa ikigharimia ka kiasi kikubwa mafunzo ya mifugo kwa wagani ili wakasimamie sekta ya mifugo. Kazi hiyo kwa sasa inatekelezwa na Wakala na sekta binafsi. Serikali kuu itabaki na jukumu la kutoa miongozo na sera zinazohusiana na uendeshaji wa sekta ya mifugo nchini. Wote tunajua umuhimu wa mafunzo kwa maendeleo ya Taifa hili na Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi mbalimbali za utoaji wa mafunzo hapa nchini kwa Taasisi za Umma na za binafsi.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi ilitoa ahadi Bungeni ya kupunguza pengo la wagani 11,303 wa mifugo wanaohitajika vijijini hivi sasa. Nina furaha kuwa ahadi hiyo tutaweza kuitimiza katika muda muafaka. Ujenzi wa majengo ya Bweni linaloweza kuchukua wanafunzi 56 na Ukumbi unaoweza kutumiwa na wanafunzi 100 kwa wakati mmoja katika kituo cha Mabuki kunafanya Wakala wa mafunzo (LITA) kuongeza uwezo wa kudahili wanafunzi 2,300 kwa mwaka. Ongezeko la idadi ya wanafunzi katika Kampasi za LITA kutasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza pengo la wagani lililopo ili kufikia lengo la kuwa afisa ugani mmoja wa mifugo kwa kila Kata na kila Kijiji.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, Serikali ilianzisha Wakala wa Mafunzo ya Mifugo ikitegemea mambo kutoka kwenu ikiwa ni pamoja na kupunguza matumizi ya Serikali. Kwa sababu hiyo, naomba kutoa nasaha zangu kwa Jumuiya ya Chuo kwa ujumla kama ifuatavyo:

§ Chuo kiendeshwe kibiashara kwa kuanzisha miradi ambayo tazalisha na kujiendesha kwa faida. Natambua kuwa mafunzo ya mifugo yanahitaji kuwa na aina mbalimbali za wanyama kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo. Kwa mtazamo huo ni budi kufuga na kutunza wanyama katika kiwango cha hali ya juu ili wanafunzi waweze kujifunza kuwa ufugaji kibiashara unawezekana na kuwa unaqweza kupunguza umasikini na kuchangia Pato la Taifa.

 

§ Uongozi wa Chuo ujitahidi kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa ujumla ili kuendana na taaluma inayotolewa. Aidha, ni vyema Chuo kikajipanga kuanza mchakato wa kuandika miradi mbalimbali ambayo inaweza kufanywa kituoni. Miradi hiyo itaweza kuwasaidia kupunguza utegemezi wa ruzuku toka Serikalini.

 

Ndugu Mkuu wa Mkoa, pamoja na kutoa mafunzo ya mifugo kwa wagani, lakini pia kituo hiki cha LITA wakishirikiana na TALIRI watafute mbinu ya kuendelea kutoa mafunzo kwa wafugaji wanaozunguka eneo hili la Mabuki. Hapa nigeomba uongozi wa Mkoa wa Mwanza na mikoa ya jirani kupiita Halmashauri zao kukaa pamoja na Uongozi wa Taasisi hizi mbili kuona namna Wilaya zitakavyoweza kutumia miundombinu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Taasisi hizi katika kuwahudumia wafugaji. Nina imani wafugaji wetu wakipatiwa stadi za ufugaji bora wa mifugo  wataweza kuinua kipato chao na Taifa kwa jumla. Ninapenda kusisitiza kuwa utoaji wa mafunzo kwa wafugaji uwe ni wa kudumu kwa kuwa hii ni njia rahisi ya kuwafikia walengwa.

 

Aidha, ningependa kuwaasa watumishi wa Taasisi hizi na watu wengine wote mlio hapa kuwa UKIMWI ni janga kwa Taifa letu. Ugonjwa huu umepunguza sana nguvu kazi ya Watanzania kwa kuathiri rika zote. Nawataka wote mzingatie maadili mema na ushauri wa wataalamu wa afya na viongozi wa Dini ili tuweze kuondokana na janga hili kwani utashi wa kuepukana na ugonjwa huu uko mikononi mwa kila mmoja wetu.

 

Wageni waalikwa, mabibi na mabwana, naomba nihitimishe kwa kutoa shukrani kwa uongozi wa Mkoa wa Mwanza, COSTECH na wadau mbalimbali kwa kuendelea kushirikiana na TALIRI na LITA ili Taasisi hizi ziweze kufanya utafiti na kutoa mafunzo kwa wanafunzi na wafugaji. Aidha, nawatakia kila la kheri watafiti, wakufunzi, Wafanyakazi, Wanachuo na Jamii yote inayozunguka Taasisi za Mabuki katika kazi zenu za kila siku.

 

Kwa kumalizia napenda kuwatakia safari njema wageni wote waalikwa mliofika kwenye uwekaji wa mawe ya mzingi katika majengo haya ya TALIRI-Mbuki na LITA-Mabuki pamoja na uzinduzi wa Kituo cha Mafunzo ya Mifugo. Mungu awaongoze ili msafiri salama na kuzikuta familia zenu zikiwa salama.

 

Kwa pamoja tunaweza, kila mtu atimize wajibu wake.

 

ASANTENI KWA KUNISIKILIZA
Axact

Post A Comment: