HAPA TIMU ZIKIKAGULIWA NA MGENI RASMI, TIMU HIZO ZILITOKA SARE YA GOLI 1-1












Mashindano ya UMISETA, kwa Mkoa wa Mwanza yamefunguliwa rasmi hapo jana na Kaimu katibu Tawala mkoa wa Mwanza Ndaro Kulwijira huku akiwaasa vijana hao wa Sekondari kucheza kwa kuzingatia nidahamu ya hali ya juu.

Zaidi soma katika Hotuba yake aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa michezo hiyo.
 

HOTUBA YA KAIMU KATIBU TAWALA WA MKOA WA MWAZA     WAKATI WA KUFUNGUA MASHINDANO YA NGAZI YA MKOA YA MICHEZO YA SHULE ZA SEKONDARI TANZANIA (UMISSETA) NSUMBA SEKONDARI TAREHE 22 MEI, 2014

Katibu Tawala Msaidizi  wa Mkoa Elimu  - Mwalimu Hamis Maulid

MaafisaElimu wa Halmashauri

Mameneja

Viongozi wa Vyama vya Michezo Mkoa

Wanamichezo

Ndugu Wananchi; na

Wapenda Michezo Wote.

 

Napenda kuchukua fursa hii kukushukuru Katibu Tawala Msaidizi ambaye ni AfisaElimu wa Mkoa, na Viongozi wenzako katika Seksheni ya Elimu kwa kunialika kufungua Mashindano haya ya Umoja wa Michezo ya Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA).

 

Nimeupokea mwaliko huu kwa furaha kwa vile umenipa fursa ya pekee kuwaona na kuzungumza na hadhara hii ya Wanafunzi Wanamichezo na Walimu wao. Aidha, nitumie fursa hii kuupongeza Uongozi wa Nsumba na jumuia yote kwa maandalizi mazuri ya mazingira kwa ajili ya mashindano haya. Ahsanteni sana!

 

Ndugu Viongozi na Vijana Wanamichezo,

Leo tumebahatika kujumuika hapa kupitia Utamaduni wa Michezo. Kwa utaratibu huu, ni dhahiri kwamba tunapata nafasi ya kujenga Umoja wa Kitaifa wa Wanamichezo kupitia Michezo hii ya UMISSETA kuanzia ngazi ya Vijana wetu wa Shule za Sekondari. Ni kweli kwamba Michezo ni Burudani, lakini kwa sasa kutokana na mabadiliko ya Mazingira ya Kisiasa, Kiuchumi na Kijamii, Michezo ni Kipaumbele katika kutoa pia Ajira kwa Vijana wetu, kukuza Biashara na kujenga jamii bora yenye maelewano. Kwa mfano, Nchi za wenzetu za Ulaya na Marekani, Nigeria, Togo, Ivory Coast, Cameroon zinatumia kikamilifu nafasi hii ya Michezo kujitangaza Kisiasa na Kiuchumi.

 

 

Ndugu Wanamichezo,

Natambua kwamba ninyi ni Wanafunzi ambao mnahitaji kukuza Taaluma na Vipaji vyenu. Moja ya nafasi hizo ni Michezo. Ili Michezo iendelee kukua Nchini, ni lazima Ukuzaji wa Vipaji vya Michezo uanzie Mashuleni. Ndiyo maana Michezo ni sehemu ya Mtaala wa Masomo yenu. Kama ambavyo tunawataka mfanye bidii sana katika masomo yenu, fanyeni bidii pia na kukuza Vipaji vyenu katika Michezo mbalimbali.

Ndugu Wanamichezo,

Michezo inatufundisha Ushindani wa Kistaarabu, Ushindani unaozingatia Sheria na Kanuni, Ushindani unaojenga urafiki badala ya uhasama; Ushindani unaoleta Upendo badala ya Chuki na Ushindani unaoleta Amani badala ya Shari. Kwa sababu hiyo Mwanamichezo wa leo anayo nafasi ya kupata mafundisho muafaka na hazina ya uzoefu mkubwa wa Ushindani wa Kistaarabu kutoka kwenye Michezo, vitu ambavyo vinaweza kumfanya kuwa Mtanzania bora wa kesho. Mwanamichezo anakubali ama Kushindwa au Kushinda. Waswahili husema“Asiyekubali Kushindwa Si Mshindani”.

Wanamichezo bora ni Watu Wasikivu, wenye nidhamu na Watiifu. Ninyi Vijana ambao ndio Viongozi wa kesho wa Taifa letu mnahitaji sana kujijengea nidhamu na maadili ya hali ya juu ili muweze kuendana na hali ya maisha ya ushindani yatakayokuwa yanawakabili. Nidhamu, inamuwezesha Mtu kufanya kazi zake kwa mpangilio mzuri unaofuata Taratibu zote za kazi kwa wakati. Hii ndiyo njia ya uhakika ya kufikia malengo yoyote yale na kupata mafanikio.

Aidha, kwa njia ya Michezo, nidhamu Shuleni itaongezeka na matarajio yetu ni kuwa nidhamu hiyo itajitafsiri pia katika matokeo mazuri kwenye Taaluma. Matarajio ni kuwa, Wanafunzi watakuwa na mahusiano mazuri zaidi kati yao na Walimu wao na wale wote wanaopata Burudani ya Michezo. Ama tunatarajia kuwa wataendelea kuwa Watu wenye Nidhamu katika Utu Uzima wao, ili hatimaye tuwe na Taifa la Watu wenye nidhamu ya kutolewa mfano.

Ndugu Wanamichezo,

Tangu zama za kale Michezo ilikuwa ni sehemu ya Maisha ya Jamii. Jamii moja ilijipambanua na Jamii nyingine kutokana na ushupavu na ushujaa wake katika Michezo. Dhana hiyo ya kale bado inaendelezwa kupitia Sera ya Michezo kwa njia ya kisasa zaidi. Sera ya Maendeleo ya Michezo inayaainisha madhumuni ya Michezo wakati huu kuwa ni:  Kujenga na kuimarisha Afya Bora kwa wote;  Kujenga Tabia ya Ushirikiano, Upendo, Undugu na Uzalendo;  Kujenga Uhusiano, Uelewano na Mshikamano Kitaifa; Kujenga Moyo wa Kishujaa na Kujihami na Kukuza Ukakamavu, Ujasiri na Kujiamini; Kuburudisha;  Kulitambulisha na kulitangaza Taifa letu nje ya Mipaka yake; na

 Kumjenga Mwanamichezo kuwa mtu imara Kiakili na Kiroho (kuanzia Utotoni hadi Utu Uzima). Kwa mtiririko huu, napenda kusisitiza kuwa Shule zote, kuanzia za Awali, Msingi, na Sekondari, viwe na Viwanja vya Michezo mbalimbali. Hii ni njia ya kuwatambua na kuwaendeleza Vijana wenye Vipaji Maalum ili hatimaye Washiriki kwenye Mashindano ya Kitaifa na Kimataifa. Aidha, Halmashauri zetu za Miji, Manispaa, Vijiji zihakikishe kuwa maeneo yaliyotengwa kwa Shughuli za Michezo yanatumika kwa shughuli hiyo. Aidha, Viwanja vilivyopo viimarishwe na vitunzwe ipasavyo.  Ndugu Wanamichezo,

Nitumie fursa hii pia kuwakumbusha kwamba mnapofurahia kushiriki katika Michezo hii, ni lazima mkumbuke pia kuwa furaha yenu itaweza kudumu kama mtatambua kuwa kuna mpinzani mkubwa kati yenu aitwaye Virusi vya UKIMWI na UKIMWI. Kila mmoja wenu anaelewa vya kutosha juu ya Adui huyu. Ni wajibu wangu kama Kiongozi na Mlezi wenu kuwakumbusha juu ya hatari inayowakabili msipochukua tahadhari ya kutosha. Kumbukeni UKIMWI bado unaenea kwa kasi kubwa sana hasa miongoni mwa Vijana wa Rika lenu kuliko Rika lolote jingine. Niwakumbushe kwamba kataeni kumalizwa na Ugonjwa huu. Msikubali kukatishwa masomo na msikubali kutenganishwa mapema na Familia zenu. Kwenu ninyi, njia bora pekee ni kusubiri hadi wakati muafaka wa kuwa na ndoa zenu. Wekeni bidii katika masomo, kwani muda ukifika yote yatajipanga vizuri.

 

Nitumie fursa hii kuwakumbusha kuepukana na matumizi ya dawa za kulevya  kama vile bangi, mirungi na cocaine kwa imani ya kuwa dawa za kulevya huwapatia nguvu  na mzuka wa kushindana, huko ni kujidanganya.  Vijana wengi hasa wanamichezo waliojaribu kutumia dawa za kulevya michezoni wameathirika na wamekuwa mataahira. Shirikisho la vyama vya michezo duniani limekataza kabisa matumizi ya dawa hizo na ukigundulika ni kufungiwa maisha na ushindi kunyanganywa. Nawaomba walimu na wanafunzi kuwabaini wale wote watakaojihusisha na utumiaji wa dawa za kulevya na kuwachukulia hatua kali za kiidhamu na kisheria

 

Ndugu Wanamichezo,

Nimeelezwa kuwa baada ya Michezo hii yapo Mashindano ya Kanda ya Ziwa ambapo Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu hukutana ili kuimarisha mahusiano ya Vijana wa Shule za Sekondari na kuunda timu moja ya Kanda. Ni muhimu Timu zetu zijipange kushiriki vizuri na kutuletea undindi a kishindo. Ni Vizuri sasa Timu hizo ziandaliwe vizuri ili zikashiriki kama Washindani na si Wasindikizaji.Kushiriki kwetu kunatujengea umahiri katika kujenga upeo wa akili za Vijana wetu na kujenga mahusiano mazuri ya kikanda .Natoa rai kwa Mashirika, Vyama vya Michezo na watu wengine  kushiriki kwa  kuchangia kufanikisha ushindi wa timu zetu za Mkoa.

 

Ndugu Wanamichezo,

Mwisho napenda kukumbusha kuwa umahiri katika jambo lolote lile hufikiwa kwa kujifunza na kufanya mazoezi mengi, kwa bidii. Napenda kuwapongeza Walimu na Waamuzi na wote walioziandaa Timu hizi ambazo leo zinashindana hapa. Nawapongeza sana Wanamichezo wa Timu zilizoteuliwa kushindana hapa. Natumaini mliteuliwa kwa kustahili na katika Michezo hii mtapata nafasi ya kuonyesha kuwa kuteuliwa kwenu hakukuwa kwa Bahati. Onyesheni Umoja, Onyesheni Upendo, na Onyesheni“Fair Play” katika mashindano haya. Kumbukeni kwamba Michezo ni Afya, Michezo ni Furaha na Michezo ni Ajira.

 

Ndugu Wanamichezo, Wageni Waalikwa,

Baada ya kusema hayo, napenda sasa nitamke kuwa,Mashindano ya Umoja wa  Michezo Shule za Sekondari UMISSETA  kwa mwaka 2014 yamefunguliwa rasmi.

Ahsanteni kwa Kunisikiliza

 

 

 

 
Axact

Post A Comment: