Uga wa Mkufunzi:Somo: Uongozi kutoka kwenye Mambo ya Kipuuzi; sehemu ya pili

Uadilifu/Unyoofu ama kwa lugha ya Kiingereza intergrity ni sifa ya ndani ya msingi ya kiongozi. Intergrity ni neno lenye asili ya Kilatini na hutokana na neno “interger” ambalo humaanisha “One=Moja” au “Wholeness=Ukamilifu” (Kwa tafsiri isiyo rasmi)… 

Mwandishi James Kalekwa

Kwahiyo basi twaweza kugundua kwamba uadilifu ni ile tabia ya kuwa thabiti na msimamo mmoja juu ya jambo fulani. Ni tabia ambayo imejijenga juu ya maneno haya “Ndiyo yenu na iwe ndiyo…”.

Kutobadilika badilika ama kwa maneno mepesi ni kutokuwa na kigeugeu!

Mtu asemaye ndiyo kwa maneno na hapana kwa matendo yake juu ya jambo hilohilo huyo si kiongozi! Lakini pia kuna watu husema ndiyo kwa maneno na matendo katika nyakati fulani au wakiwa na watu fulani na kisha husema hapana kwa maneno na matendo juu ya jambo hilihilo katika nyakati na wakiwa na watu tofauti na wale awali. 
Hawa nao so viongozi! Kwa kifupi uadilifu ni kukiishi kwa maneno na matendo kwa kutokubadilika kile unachokiamini. Hilo ni jambo la kwanza!

Nakumbuka Mfalme Suleimani mwenye hekima husema “Aendaye kwa unyofu (uadilifu) huenda salama….”.

Walimwengu mlioko Tanzania mtakuwa mnakumbuka vyema juu ya Azimio la Arusha la 1967 ambalo lilihimiza na kusimamia uadilifu kwa viongozi wa chama na serikali na nyote ni mashahidi kwamba wasiokuwa na moyo wa uongozi walijikuta nje ya mstari. Kisha likafuatia Azimio la Zanzibar ambalo lilikuwa ni kaburi la Azimio lililotangulia!

Ni mara ngapi umeshuhudia “viongozi” wakivunja miiko na maadili ya uongozi kwa kusema uongo hadharani bila woga wala aibu- tena uongo unaosindikizwa na tafiti na taarifa za kitakwimu ili kujipatia faida fulani?

Walimwengu, mnakumbuka hadithi ya Samsoni na Delilah? Samsoni alichimba kaburi ambalo lingemzika yeye mwenyewe baada ya kuanza “kuona asiyopaswa kuyaona, kwenda ambako hakupaswa kwenda na kutenda ambavyo hakupaswa kutenda” – yaani alivunja miiko mahsusi kwaajili yake na aina ya ungozi wake…
 Alianza taratibu kuingia katika mahusiano ya kimapenzi (ufuska) na hatimaye alijikuta mikononi mwa Delilah na ndipo ndoto zake zikazima (Alitobolewa macho kama ishara ya kifo cha maono/malengo/ndoto yake) na hadithi ikaishia hapo! “Viongozi” wengi hujikuta wameanza kuasi maadili na miiko taratibu (huanza kwa kula rushwa kidogo, kusaliti kidogo, kudanganya kidogo) na hatimaye hukubuhu!

Pili, uadilifu ni kujisikia deni ama kuwiwa kuwajibika au kuwa mkweli juu ya maneno yako. Kuna usemi usemao “Ahadi ni deni” …

 Je, ni mara ngapi umeshuhudia “viongozi” wakitoa ahadi lukuki ambazo hawazitimizi? Ama huja na kukurubuni ukubaliane nao kwamba wamezitimiza (kwa namna waonavyo wao)?-
 Kumbe ki uhalisia hawajatimiza! Walimwengu, Je, mtu anayeahidi kutenda jambo fulani na asitende au kuyakana maneno aliyoyasema awali akiwa mahali fulani mwaweza kumtegemea na/au kuyaamini ayasemayo? La hasha!

Kuna mamia kwa maelfu ya viongozi waliokufa na kwenda kaburini na madeni (ahadi ambazo hawakuzitimiza) kibao! Wapi na ni lini wataenda kulipa baada ya kifo?

Jambo la tatu na la msingi juu ya uadilifu ni ukweli/uaminifu. Wengi huutazama ukweli/uaminifu kama “hali ya kutoshiriki kusema uongo au udanganyifu”.

Lakini ningependa kwenda hatua kubwa zaidi ya hapo kwasababu katika jamii yetu kwa sasa “viongozi” huelezea mambo na kuyatia chumvi katika kuelezea uzuri au ubaya wa jambo husika. Ukweli/Uaminifu ni ni hali ya kuuwasilisha uhalisia kwa kadri inavyowezekana kwa dhamiri safi na kuepuka uwasilishaji ambao hitimisho lake ni udanganyifu. The Joseph Institute of Ethics inaueleza ukweli/uaminifu

“Ni kuepuka uwasilishaji usio sahihi wa uhalisia. Inawezekana kabisa kuwasilisha mambo mengi ya ukweli ambayo humshawishi msikilizaji kuamini vitu visivyo sahihi. 
Hivyo mtu anaweza kuzungumza ukweli pasipo yeye kuwa mkweli. Kwasababu amekuwa na dhamira ya kumfanya mtu afikie hitimisho ambalo si la kweli…. Ni dhamira, nia ama kusudi la mtu…”

Walimwengu wenzangu, mimi nimeshuhudia watu wakisema umri tofauti na umri wao halisi hasa katika michezo na mahusiano kwa nia ya kupata wanayoyahitaji. 
Nimeshuhudia wasomi na wataalamu wakiunda “cook” tafiti, miradi na taarifa mbalimbali vyumbani mwao ili wapate hitaji lao. Nimeona wengi wakigushi risiti na karatasi za kufanyia malipo ili mkono uende kinywani.

Wapendwa walimwengu, hasa mlioko Tanzania, mmewahi kusikia juu ya TAKRIMA? bila shaka mmejionea na/au kusikia wengi wakipewa bahasha za kaki, wengine wakitoa vitu kama mavazi (t-shirt, khanga, kofia, vitambaa n.k) na chakula si kwa upendo bali kwa nia ya kulaghai. 
Mmeshuhudia watu wakizunguka huku na kule wakitoa/wakigawa fedha kwa nia ya kushawishi? Hoja ninayojenga hapa ni kwamba mtu anaweza kutenda mambo yanayoonekana ni mema kwa nia mbaya! Hawa si viongozi hata chembe! Kila asomaye na afahamu.

Nikiwa katika mwaka wangu wa mwisho katika elimu yangu ya sekondari nilikutana na msemo usemao “Asiyejua aendako, ataenda kokote.”…

Miaka kadhaa baada ya kuutafakari niliutengenezea swali ambalo huwa napenda kuwauliza vijana, vikundi na jumuiya, watu walio katika mahusiano n.k. Hebu jaribu kufikiri umemsindikiza ndugu yako kituo kikuu cha mabasi (stendi) na baada ya kuagana naye anatokea mtu mmoja akiwa na mizigo na kwa kumtazama unagundua kuwa ni msafiri na anahitaji masaada.

Huyu msafiri anakufuata na kukuomba umuonyeshe basi (gari la abiria) ili aweze kusafiri. Kwa akili za kawaida, kabla ya kumuonyesha basi ungependa kujua anaelekea wapi (mwisho wa safari yake) ili ujue basi la kumwelekeza. Lakini cha ajabu msafiri huyo anakujibu ya kuwa “Sijui ninataka kwenda wapi…”; 
Je, utamwonyesha basi gani/la kwenda wapi?.... Asiyejua aendako ataenda kokote! Huwezi na ni uendawazimu kuanza safari wakati hujui unaenda wapi. Lazima uujue mwisho wa safari ndipo uianze safari.

Walimwengu wenzangu, jamii yoyote inahitaji kujua inakwenda wapi. Ni jukumu la lazima la kiongozi kujua, kuona na kuielekeza jamii yake kwenda mahali inapopaswa kwenda- HATMA! Je, twaukumbuka mfano ule wa kipofu kumwongoza kipofu mwenzake? Wote huishia shimoni. 
Hivyo ni jukumu la mwongozaji kuwa ni mtu anayeona kule jamii inapaswa kwenda. Uwezo wa kuwa na Maono (Vision), Malengo (Goals) ama Hatma (Destiny) ni lazima kwa kiongozi.

Nikirejea hekima za Mfalme Suleimani asemapo “Pasipo maono/malengo watu huangamia/ hukosa kuwa na adabu…”

(Mkolezo unaonyesha tafsiri zingine) nawiwa kusema kwamba kiongozi ni mtu mwenye uwezo wa kuona mwisho kabla ya mwanzo, kuwaeleza wanajamii juu ya mwisho huo na kuwashawishi kwenda pamoja naye katika mwisho huo huku akiongoza njia! Wapendwa wangu walimwengu,

Je, mkitazama katika jamii zenu mnaona watu wenye uwezo huo? Nazungumza katika Nyanja zote. Niwakumbushe tu kwamba ni muhimu tukitambua kwamba malengo/hatma/maono hayaigwi wala kunakiliwa kwani kuna maono mahsusi kwa kila jamii husika.
Axact

Post A Comment: