TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella, amewaapisha wakuu wapya wa  Wilaya za Mkoa wa Mwanza na kuwapa vitendea kazi ikiwapo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Ilani ya Chama Tawala Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2015- 2020, kwaajili ya kwenda kutimiza wajibu wao wa Kikatiba kwenye wilaya walizo pangiwa.

Akizungumza baada yakuwaapisha, Mhe. Mongella, amewataka waende wakasimamie shughuli za maendeleo, kuhimiza suala la ulinzi na usalama kwenye Wilaya zao, huku akitilia mkazo ukomeshwaji wa  mauwaji ya watu wenye Ulemavu wa Ngozi Albino pamoja na Vikongwe, amesema, ikiwa jamii ya watu hao itapata madhara basi ni dhahiri Mkuu huyo wa Wilaya husika atakuwa ameshindwa kusimamia majukumu yake.

Mkuu huyo wa mkoa pia, amerudia kauli yake nakuwataka viongozi hao wapya watambue wanajukumu zito lililoko mbele yao, ikiwa ni pamoja na kukomesha Utumiaji wa dawa zakulevya.

 

Aidha ameonya  uchezaji wa  Pool na unywaji wa  Pombe wakati wa saa  kazi, huku akimsisitiza mkuu wa Wilaya ya Nyamagana kuhakikisha ifikapo Agosti mosi, suala la wafanya biashara wanaofanya biashara kwenye maeneo ambayo hayaruhusiwi liwe limepatiwa ufumbuzi.

Mongella amesema, katika Mkoa wa Mwanza, Hotel na Klabu, yeyote ile, iwe ya kawaida au ya Kitalii, ikibainika inafanya biashara ya Shisha, hawata ivumilia na badala yake wataifutia Leseni ya biashara.

 

Walio apa mbele ya Mkuu wa Mkoa, ambao waliteuliwa na Mhe. Rais Tarehe 26, Juni, 2016  ni Emmanuel Enock Kipole, Mkuu wa Wilaya ya Sengerema,   Estomin Francis Chang’a Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe,  Hadija Rashid Nyembo Mkuu wa Wilaya ya Magu, wengine ni Juma Samwel Sweda Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Dkt. Leonard Moses Masale Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Mary Onesmo Tesha Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana na Mhandisi Mtemi Msafiri Simioni Mkuu wa Wilaya ya Kwimba.

 

Imetolewa na

Atley J. Kuni

Afisa habari na Mahusiano

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

MWANZA.                                                                                          04, Julai, 2016.

 

 
Axact

Post A Comment: